Mkuu wa Mkoa wa Simiyu Azindua mradi wa ukarabati wa Bwawa la Nyangokolwa
Zaidi ya wananchi 3,000 wa Wilaya ya Bariadi mkoani Simiyu
wanatarajia kunufaika na huduma ya uhakika ya maji baada ya Serikali
kuzindua mradi wa ukarabati wa Bwawa la Nyangokolwa wenye thamani ya
takribani Shilingi bilioni 1.012.
Mradi huo umezinduliwa na Mkuu
wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anamringi Macha, huku usimamizi wa utekelezaji
ukifanywa na Bodi ya Maji Bonde la Ziwa Victoria kupitia wataalamu wake.
Akizungumza
wakati wa uzinduzi huo, Mhe. Macha ameipongeza Bodi ya Maji Bonde la
Ziwa Victoria kwa usimamizi mzuri wa rasilimali za maji na utekelezaji
wa miradi mbalimbali ya mabwawa katika Mkoa wa Simiyu, akieleza kuwa
miradi hiyo inaendelea kuboresha maisha ya wananchi.
Aidha,
amewataka wataalamu kuhakikisha mradi huo unakamilika ndani ya muda
uliopangwa na kwa viwango vinavyotakiwa, huku akisisitiza kuwa
ataufuatilia kwa karibu hadi utakapokamilika.
Kwa upande wake,
Naibu Waziri wa Maji ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Bariadi Mjini,
Mhe. Mathew Kundo, amesema ukarabati wa Bwawa la Nyangokolwa utakuwa
chachu ya maendeleo ya kiuchumi kwa wananchi kupitia upatikanaji wa maji
kwa shughuli za kilimo, umwagiliaji na ufugaji.
Ameeleza kuwa
mradi huo ni matokeo ya dhamira ya Serikali ya Awamu ya Sita chini ya
uongozi wa Mhe. Dkt Samia Suluhu Hassan ya kuhakikisha wananchi wanapata
huduma bora za maji.
“Sisi
wananchi wa Nyangokolwa tunamshukuru sana Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu
Hassan kwa kuona umuhimu wa ukarabati wa bwawa hili. Mradi huu utaondoa
changamoto ya uhaba wa maji na kuboresha maisha ya wananchi,” amesema
Mhe. Kundo.
Akitoa taarifa ya utekelezaji wa mradi huo,
Mkurugenzi wa Bodi ya Maji Bonde la Ziwa Victoria, Dkt. Renatus Shinhu,
amesema baada ya kukamilika, bwawa hilo litakuwa na uwezo wa kuhifadhi
lita za ujazo milioni 12 za maji, na kunufaisha zaidi ya wananchi 3,000
pamoja na mifugo zaidi ya 5,000.
Dkt. Shinhu ameahidi kuwa Bodi
ya Maji Bonde la Ziwa Victoria itasimamia utekelezaji wa mradi huo kwa
weledi ili ukamilike kwa wakati na kuzingatia viwango vyote vya ubora
vinavyotakiwa.
Wananchi wa Nyangokolwa waliohudhuria uzinduzi huo
wameishukuru Serikali kwa kuanza ukarabati wa bwawa hilo, wakisema kwa
muda mrefu wamekuwa wakikabiliwa na uhaba wa maji uliowaathiri katika
matumizi ya nyumbani, shughuli za uzalishaji na ufugaji, hali
iliyowalazimu kutembea umbali mrefu kutafuta maji.
Uzinduzi wa
mradi huo umehudhuriwa na viongozi kutoka Wizara ya Maji, Mkoa wa
Simiyu, Wilaya ya Bariadi, wataalamu wa Bodi ya Maji Bonde la Ziwa
Victoria pamoja na wananchi wa eneo hilo, ambao wameeleza matumaini
makubwa kuwa mradi huo utaleta suluhisho la kudumu la upatikanaji wa
maji na kuchochea maendeleo ya kijamii na kiuchumi katika Wilaya ya
Bariadi.